Saturday, November 21, 2009

Kilimo Kwanza inavyoendelea kuzua majambo!

Wanawake 26 wakazi wa kijiji cha Ndolezi wilayani Mbozi mkoani Mbeya jana waliandamana umbali wa kilometa 30 kwa miguu hadi ofisi ya mkuu wa wilaya ya Mbozi kupeleka madai ya kunyimwa mbolea ya ruzuku.

Kiongozi wa wanawake hao Mary Anyangalile ameliambia gazeti hili kuwa Afisa Mtendaji wa kijiji chao amewanyima mbolea na kuwapa wanaume kwa madai kuwa wanawake hawastahili kupewa mbolea hizo. Aidha aliongeza kudai kuwa mgawo wa mbolea hizo unaotolewa kwa upendeleo umewapa vijana wadogo ambao hawana nyumba (hawajaoa) na hivyo kuwafanya wao waamini kuwa kuna mazingira ya rushwa.

Linas Hebron, mmoja wa wanawake hao alieleza kuwa kaya nyingine zimepewa hadi mifuko 4 ya mbolea ili hali wao hawakupata na kwamba hawastahili kupata ndiyo maana wanataka kumwona mkuu wa wilaya awasaidie watambuliwe na kupewa mbolea hizo.

Walalamikaji hao ambao waliandikiwa barua na diwani wa kata ya Mlangali Juma Mnkondya ya kupeleka kwa mkuu wa wilaya hawakufanikiwa kumwona kwa kuwa ilikuwa Jumamosi siku ambayo ni ya mapumziko na hivyo barua yao kupokelewa na afisa tawala aliyejulikana kwa jina moja la Kikosa.

Afisa Mtendaji wa kijiji cha Ndolezi Elia Kalinga alipohojiwa juu ya malalamiko hayo ya wanawake alidai kuwa yeye anawapa wanaume kwa kuwa ndiyo wakuu wa kaya na iwapo wanawake wayo mashamba yao hana mwongozo wa kuwapa mbolea hizo.

Mkuu wa wilaya ya Mbozi Gabrieli Kimolo aliwaambia waandishi wa habari mwishoni mwa wiki kuwa wakulima wana uelewa mdogo juu ya suala la mbolea za ruzuku na hivyo kujiona kuwa wote wanastahili kupata mbolea hizo na ndiyo sababu ya kuwepo kwa migogoro inayoendelea hivi sasa wilayani hapa.

Uchunguzi wangu umebaini kuwepo kwa njama za makusudi za baadhi ya watendaji wa vijiji kujinufaisha kwa kuhodhi baadhi ya vocha za pembejeo na kuziuza kwa mawakala wa usambazaji wa pembejeo. Zoezi la ugawaji wa pembejeo za ruzuku umeingia dosari baada ya kubainika kuibiwa vocha za sh milioni 86 katika ofisi ya kilimo ya wilaya ambapo watuhumiwa wameshafikishwa mahakani.

Uchunguzi zaidi unaonesha njama nyingine za baadhi ya wahusika kuwazunguka viongozi wa vijiji na kuwasainisha hati za mapokezi ya vocha kwa idadi isiyolingana na mapokezi halisi na hivyo kuwatia kitanzini watendaji hao iwapo serikali itafuatilia na kuhakiki mapokezi hayo.
mwisho

Thursday, November 19, 2009

Watumishi watano wa halmashauri ya wilaya ya Mbozi wamepandishwa kizimbani kujitu tuhuma za wizi wa vocha za pembejeo zenye thamani ya shilingi milioni 86.

Watumishi hao ni Joseph Mbogela (59) afisa kilimo, Asante Ndimbo (46) afisa kilimo na Tekla Luoga (54), wengine ni Maiko Mwashiuya (45) dereva, Goodluck Mbazu (33) dereva na Richard Mnkondya (41) mfanyabiashara aliyepatikana na vocha mali ya wizi zenye thamani ya shilingi milioni 25.

Watuhumiwa wote ambao walishitakiwa mbele ya hakimu wa mahakama ya wilaya Nyasige Kajanja wamekana mashitaka yaliyosomwa dhidi yao na mwendesha mashitaka wa polisi Charles Makunja.

Kesi itatajwa tena Disemba 5, washitakiwa wamepewa dhamana ya maneno ya shilingi milioni 5.

Site search

    More Text