Monday, March 8, 2010

Jinsi Camartec ilivyo jizatiti kuokoa misitu kwa kusambaza teknolojia ya matumizi ya gesi itokanayo na wanyama
• CARMARTEC yatua Mbozi

• Yaja na aina mpya ya mtambo wa gesi uitwao CAMARTEC MODIFIED DESIGN

• Vijana kunufaika na ujenzi

• Wateja kujengewa kwa 2/3 ya bei



Wananchi wilayani Mbozi mkoani Mbeya wameshauriwa kuanza ufugaji wa kisasa ambao kwa kutumia teknolojia ya gesi ya wanyama utapunguza ukataji miti na kuiokoa nchi kwa janga la ukame.



Wito huo umetolewa na kaimu Mkurugenzi Mtendaji wilaya ya Mbozi Afwilile Lamsi alipofungua mafunzo ya siku 10 yanayotolewa na kituo cha zana za kilimo na teknolojia vijijini (CAMARTEC) kwa mafundi waashi ya namna ya kujenga mitambo ya gesi.



Lamsi aliongeza kuwa wilaya ya Mbozi kwa hivi sasa ina watu zaidi ya 600,000 ambao wanahitaji kubadilisha ufugaji kutoka ule wa kuchunga mbugani na kulishia ndani hali itakayofanya upatikanaji wa nishati ya gesi kuwa rahisi na hivyo kuokoa mazingira.



Awali Afisa Mkuu wa Mafunzo wa CAMARTEC Harold Ngowi akimkaribisha mkurugenzi kufungua mafunzo alisema kuwa kituo chake kinatoa mafunzo hayo na kuendesha mradi wa gesi kwa hisani ya shirika la maendeleo la Uholanzi (SNV) likiwa mshiriki mkuu.



Ngowi aliongeza kuwa lengo ni kujenga mitambo mitambo 12,000 katika miaka 5 ya mradi ambao ulianza Novemba 2008 na ambao hadi sasa umejenga mitambo 165 na kufundisha mafundi 180 katika mikoa ya Tanga, Arusha, Iringa, Kilimanjaro, Manyara na Pwani.



Aidha Ngowi alifafanua kuwa CAMARTEC wamebuni aina mpya ya mtambo ambao ni bora zaidi ya ule wa awali uliojulikana kama CAMARTEC FIXED DOME kwa kuanza aina mpya iitwayo Modified CAMARTEC Design ambao umeelezwa kuwa ujenzi wake ni rahisi zaidi.





Kutokana na mtambo huo mpya nchi kadhaa zikiwemo Uganda, Ethiopia, Kenya na Ruanda wanakuja Tanzania kujifunza kwa kuwa ni nchi yenye uzoefu na mitambo ya biogas.



Hata hivyo mkakati huo ulianzishwa na serikali ya Uholanzi iliyoitisha mkutano mkubwa wa wadau wa technolojia ya biogas wa nchi za Afrika jijini Nairobi nchini Kenya mwaka 2007 ambao ulihudhuriwa na nchi nyingi.



Ni kutokana na mkutano huo wizara ya nishati na madini ikaitikia na kukabidhi mradi huo kwa CAMARTEC ili kuusimamia na kuuendesha kwa kusambaza teknolojia hiyo vijijini.



Mradi wa Biogas Tanzania umelenga kaya vijijini ili kuwanusuru wanawake na adha ya utafutaji kuni pamoja na kuhifadhi mazingira kwa kuinusuru miti inayokatwa kwa ajili ya nishati ya kuni na mkaa.


Wateja watakaokuwa tayari kujengewa mitambo hiyo watalipiwa gharama za ujenzi huku wakichangia kiasi kidogo cha pesa kwa ajili ya vifaa kama saruji, mabomba, taa na majiko ya gesi.


Mafunzo hayo yanatolewa huku idadi kubwa ya mafundi wanafunzi wakiwa ni wanawake ambao ni 14 na wanaume 11 ishara ya kutambua umuhimu wa teknolojia hiyo kwa wanawake. Ujenzi huo utawafanya akina mama kufanya kazi nyingine zaidi kuliko kwenda misituni kutafuta kuni

Simbeye azikwa

Posted by Unknown On 11:14 PM No comments
Buriani David Lumbala Simbeye

Katika mazishi yake yaliyohudhuriwa na viongozi mbalimbali wa mkoa wa Mbeya baada ya mwili wa marehemu kuagwa jijini Dar na Rais Jakaya Kikwete, Waziri Mkuu Mhe. Mizengo Pinda na viongozi wengine waandamizi wachungaji waliachiwa sehemu yao ya ujumbe kama hivi: 

Watanzania wameshauriwa kumchagua kiongozi anayemwogopa Mungu bila kujali dini yake katika uchaguzi mkuu wa mwaka huu.
Wito huo ulitolewa hivi karibuni na Askofu Kiongozi wa Kanisa la Moravian Tanzania Alinikisa Cheyo katika hotuba yake aliyoitoa wakati wa mazishi ya aliyekuwa Mkuu wa Kikosi cha Ulinzi wa Viongozi marehemu David Simbeye yaliyofanyika kijijini kwake Mbimba wilayani Mbozi.
Alisema mwaka wa uchaguzi umewadia ni vizuri wakachaguliwa viongozi wanaomwogopa Mungu bila kujali dini au madhehebu yao na ambao wanauwezo wa kuongoza bila ya kuangalia fedha chafu wanazogawa.

“Mwaka huu wa uchaguzi watu wanagawa fedha chafu nawe ukizipokea utakuwa mchafu na utakuwa umeuza uhuru wako kwa fedha ambayo haiwezi kukuletea maendeleo” Cheyo alisisitiza.

Hata hivyo Cheyo alidai kuwa sababu kubwa ya watu kupenda kupokea rushwa hiyo ya uchaguzi ni kutokana na vijana wengi kutokuwa na mipango thabiti ya kazi hivyo kujiweka katika hali ya uhitaji ambapo akiletewa fedha hiyo chafu hatakuwa na ujasiri wa kuikataa.

Marehemu Simbeye ambaye alifariki Februari 28, mwaka huu alizaliwa mwaka 1933 wilayani Ileje na kupata elimu yake ya msingi katika shule ya Itumba mwaka 1945-50 na baadae kujiunga na Mbozi Middle School mwaka 1951-hadi 1952.

Mwaka 1953 alijiunga na jeshi la polisi alikofanya kazi hadi 1964 alipohamishiwa Ikulu ambako amefanya kazi hadi alipostaafu 1988 akiwa mkuu wa kikosi cha ulinzi na akiwa ni mlinzi binafsi wa Mwalimu Julius Nyerere (bodyguard) baadae Rais Ali Hasan Mwinyi.

Marehemu David Simbeye alisafiri kutoka Mbozi kwenda Dar siku hiyo ya Februari 28 ambapo alifika jijini Dar majira ya saa tisa alasiri na kufikia katika hoteli na baadaye alijisikia vibaya hali iliyomfanya ampigie simu mtoto wake Leonard ambaye alifika muda mfupi baada ya mauti kumpata.
Maelezo zaidi yalitolewa na msemaji wa familia ambaye pia ni mpwa wa marehemu Henry Mgala Bantu aliyeeleza kuwa safari ya marehemu kwenda Dar ilikuwa kwa minajili ya kumwona daktari kwa maradhi ya moyo aliyokuwa akilalamika mara kwa mara.

Akiwa kijijini hapo Simbeye alikuwa anajishughulisha na kilimo cha kahawa huku akitumia usafiri wa baiskeli kumleta mjini Vwawa kama kilometa 2 ½ kupata mahitaji yake.

Mzee Simbeye atakumbukwa kwa ushauri na nasaha zake ambazo hakuacha kuzitoa kwa vijana kila mnapoonana.

"Bwana alitoa na Bwana ametwaa jina lake libarikiwe"

Site search

    More Text