Friday, August 1, 2008

Na Kenneth Mwazembe
Mbozi

MTOTO Lucia Osward mwenye miezi 9 juzi aliliwa na mamba huku mama yake Bahati Kawepo (28) mkazi wa Irambo Ivuna wilayani Mbozi mkoani Mbeya akinusurika kifo baada ya kukamatwa na mamba alipokuwa akivuka mto Momba.

Akielezea mkasa huo uliomfanya apoteze mtoto wake Lucia Osward (9/12) akiwa amelazwa katika wodi la wanawake na watoto katika hospitali ya mjini Vwawa, alisema kuwa juzi jioni saa 2 usiku akitokea kijiji cha Ivuna kusaga mashineni akiwa anavuka mto ndipo mamba alipotokea na kumng’ata sehemu za siri ambazo nusura aziondoe kabisa.

“Nilipiga kelele za kuomba msaada ndipo mume wangu alipofika na kumshika mamba ulimi na mwanamke mwingine aliyefika kutoa msaada alimshika mkia mamba wakawa wanamvutia nchi kavu ndipo aliponiachia na kuninyang’anya motto aliyakuwa mgongoni na kukimbia naye” anamalizia mama huyo.

Mama huyo alipelekwa katika kituo cha afya cha Kamsamba kwa mkokoteni uliokokotwa na ng’ombe na kupewa matibabu ya awali na kukimbizwa katika hospitali ya wilaya ambako anaendelea na matibabu.

Mganga Mkuu Egfrid Mwingirihela ameeleza kuwa majeruhi huyo alijeruhiwa vibaya sehemu za siri na kutenguka bega la kushoto na majeraha ya vidonda kichwani na miguuni na kwamba hali yake inaendelea vizuri.

Habari kutoka Kamsamba zimeeleza kuwa msako mkali unaendelea dhidi ya mamba huyo aliyemla mtoto ukishirikisha wanakijiji waishio jirani na eneo hilo .

Ziwa Rukwa linaaminika kuwa na mamba wengi kuliko samaki na hivyo kuwafanya wananchi wanaoishi jirani na ziwa hilo kuishi kwa mashaka, pengine umefika wakati wa serikali kuvuna mamba hao ili kuwapunguza au kuwafuga kitaalam na kunusuru maisha ya wenyeji.

KATIKA hospitali hiyo hiyo, jana jioni mwanamke mmoja Morina Sichone (22) mkazi wa kijiji cha Nambala wilayani hapa alijifungua kitu cha ajabu baada ya kuwa mjamzito wa miezi 8.

Akieleza mkasa huo uliovuta hisia za watu na kuhusisha kitendo hicho na ushirikina, Sichone alisema kuwa yeye alijihisi mjamzito tangu mwezi wa Novemba 2007 na kwamba alihudhuria kliniki katika hospitali ya wilaya ambako walimfungulia kadi na kuthibitisha kuwa ilikuwa mamba.

Ni miezi miwili iliyopita hakusikia kucheza kwa mtoto hadi jana alipojisikia uchungu na kufika katika wodi la wazazi ambapo alijifungua kiumbe hicho kilichokuwa kama yai ambacho alilazimika kukipeleka kwa wakwe zake ili wasijedai kuwa ameuza mtoto.

Mganga Mkuu wa hospitali hiyo Egifrid Mwingirihela amethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba bado wahawajaweza kutambua ni kitu gani kilisababisha hayo.
MWISHO



Katika tukio jingine MCHUNGAJI

Mchungaji Silas Mwamwezi wa kanisa la Moravian wilayani Mbozi wiki iliyopita alizuiwa kufungisha ndoa katika kijiji cha Mpela baada ya kubainika kuwa bibi harusi alikuwa ni mwanafunzi wa kidato cha III katika shule ya Ipunga wilayani Mbozi.

Zoezi la ufungaji ndoa baina ya Hamisi Zawadi Mnkondya na Maria Makanga (20) lilizuiwa na Kaimu Afisa Mtendaji wa Kata ya Ihanda Blaya Msongole aliyefika na mgambo hapo kanisani na kumkamata bwana harusi na kumpeleka kituo cha polisi mjini Vwawa.

Afisa huyo alieleza kuwa alipewa taarifa na Mkuu wa shule hiyo kuhusu kuozwa kwa binti huyo ambapo alilazimika kwenda na kuzuia Ibada hiyo isifanyike ambapo tayari shamla shamla zilikuwa zimeshaanza na walikuwa hatua za awali za kuvishana pete.

Aidha Msongole alisema kuwa jitihada za kumtafuta Rosta Mnkondya ambaye ni mama yake bibi harusi anatafutwa kwa tuhuma za kumuoza kwa ng’ombe mbili ilihali akijua kuwa binti yake ni mwanafunzi.

Mkuu wa shule Daniel Kasomo alipohojiwa juu ya tukio hilo alisema kuwa Maria ni mwanafunzi mtoro tangu Aprili mwaka huu alipoacha kuhudhuria masomo na kwamba alipopata taarifa za ndoa hiyo alitoa taarifa kwa uongozi.

Naye Mchungaji Silas Mwamwezi alipohojiwa juu ya yeye kufungisha ndoa na mwanafunzi alisema anasikitika kwa tukio hilo , yeye ni mchungaji wa usharika wa Vwawa makao makuu ya wilaya katika jimbo hilo na kwamba aliitwa kufungisha ndoa hiyo bila kujua kuwa kuna mwanafunzi kati ya maaharusi hao kwani kanisa lake haliruhusu wanafunzi kuolewa.

Polisi wilayani hapa wamethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kwamba bwana harusi anashikiliwa na polisi ambapo atafikishwa mahakamani mara uchunguzi ukishakamilisha.

MWISHO

0 comments:

Post a Comment

Thank you for reading the article

Site search

    More Text