Tuesday, December 30, 2008

MTOTO ANAYEHITAJI MSAADA WA KI-UTU

Posted by Unknown On 9:49 PM No comments


Mtoto Erica Laurent (1) aliyezaliwa bila njia ya haja kubwa amekuwa na tatizo la kufumuka nyuzi kila anaposhonwa katika hospitali ya rufaa Mbeya alipofanyiwa operation Novemba 2007. Baba wa mtoto Laurence Msongole amekataa kutoa fedha za matibabu, amemtelekeza mke baada ya kuzaa mtoto mwenye matatizo.

Hivi sasa mama wa mtoto Huruma Mwaijande anaishi kwa wazazi wake ambao nao wameshindwa kupata fedha za matibabu kufuatia umaskini unaoikabili familia hiyo.

Mtoto huyo amepangiwa kwenda Muhimbili kwa matibabu zaidi lakini uwezekano hauopo kutokana na ukweli kwamba familia haina uwezo hata wa kugharamia matibabu katika hospitali ya rufaa ya Mbeya.

“Tulifukuzwa katika nyumba tuliyopanga na mume wangu, tukahamia kwa mama mkwe ambaye amepanga chumba na sebule, baba na mama mkwe wanalala chumbani na mimi na mume wangu tunalala sebuleni hali iliyonifanya nihame nije kuishi kwa wazazi wangu” anasema Huruma.

Mama na mtoto huyo wanaishi mtaa wa Ilembo mjini Vwawa wilayani Mbozi, wamefika ofisi ya mkuu wa wilaya kuomba msaada, ofisi hiyo imetoa kibali ili mama huyo azunguke mitaani kuomba msaada kwa wasamaria apate fedha za kumpeleka mgonjwa Muhimbili Dar es Salaam.

Huruma anao watoto wawili, ambapo mkubwa ni Sabina Laurence (3) na Erica ambaye ni mgonjwa.

Baba ya wa mtoto Laurence Msongole alipohojiwa juu ya tuhuma za kumtelekeza mke, anasema yeye hajagoma kutoa fedha ila hana fedha hizo hata nauli ya kwenda rufaa jijini Mbeya anashindwa.
Babu wa mtoto huyo Hatson Mwaijande anasema imekuwa ni mzigo kwake kwani mkwe wake amemwachia gharama zote za kuzunguka na mtoto, hata chakula chao ni shida inabidi awasaidie kwa kuwapa mtaji wa kuuza maparachichi kwa ajili ya kujikimu.
"Mkwe wangu ni fundi uashi lakini hatoi fedha kwa ajili ya famila yake, hii inasikitisha sana" anasema kwa masikitiko Mwaijande
Mwisho.

0 comments:

Post a Comment

Thank you for reading the article

Site search

    More Text