Wednesday, March 26, 2008

Posted by Unknown On 3:22 AM No comments
a Kenneth Mwazembe
Mbozi

Wananchi wa miji ya Vwawa, Tunduma na Itaka wilayani Mbozi mkoani Mbeya wamewalalamikia watendaji serikalini likiwemo Jeshi la Polisi kwa unyanyasaji dhidi ya raia na madaraka ya watendaji wa vijiji yasiyo na mipaka.

Malalamiko hayo yalitolewa jana kwa taasisi ya Vantage Communications inayojishughulisha kukusanya takwimu juu ya matatizo ya wananchi likiwemo la urasilimishaji mali na biashara.

Awali kabla ya kuanza kupokea malalamiko hayo Mtakwimu Peter Mayeye wa Turaco Systems Consultant (T) Ltd inayofanya kazi kwa niaba ya Vantage Communications aliwatoa wasi wasi wananchi na kwamba wakitoa maoni yao hawatatajwa majina na hivyo kuwaondoa wasiwasi waliokuwa nao kabla.

Wakielezea unyanyasaji wa Jeshi la Polisi wamesema polisi wana tabia ya kuwafungulia kesi za kubambikiza wakati wowote usipokubaliana na matakwa yao, watuhumiwa kupigwa bila sababu na wengine wamesababishiwa vilema baada ya kupigwa na kuvunjwa mikono na miguu.

Wananchi wengine wamedai kuwa kusikia kuwa kutakuwa na polisi jamii lakini hawajaziona hatua za makusudi za kuwaelimisha wananchi kwa kuwa Jeshi hilo limejifanya adui wa wananchi.

Wameomba pia kuwepo chombo kinachoangalia utendaji kazi wa Jeshi la Polisi kwani mwananchi akiwa na malalamiko dhidi ya Jeshi hilo hana pa kuyapeleka kwani ukimshitaki kwa Kamanda wa Mkoa hawezi kuwachukulia hatua yoyote kwa kile kilichoelezwa kuwa ni kulindana na kulinda heshima ya Jeshi hilo.

Watendaji wa vijiji na kata pia wamelalamikiwa kwa kujichukulia hatua wasizostahili na hasa wanapodai michango ya ujenzi wa sekondari ambapo imeelezwa kuwa huwakamata wananchi na kuwafungia katika mahabusu zao huku wakilazimishwa kulipa michango na gharama za kuwakamata.

Kero nyingine iliyolalamikiwa ni zoezi zima la uandikishaji hati miliki za kimila ambapo imeelezwa na wananchi kuwa urasimu ni mkubwa na utaratibu wa gharama za picha kwa kila eneo ni mzigo usiobebeka.

Taasisi ya Vantage Communications yenye makao yake makuu Uganda ina tawi hapa Tanzania ambalo limeajiriwa na MKURABITA ili kukusanya maoni ya wananchi katika mchakato mzima wa kujua kero za wananchi hasa katika zoezi la urasilimishaji mali.

MWISHO

Friday, March 14, 2008

HOFU YAZIDI SHULE YA SEKONDARI

Posted by Unknown On 1:19 AM No comments
Na: Kenneth Mwazembe – Mbozi.

Wananchi wa Kata ya Msia wilayani Mbozi mkoani Mbeya wamesikitishwa na hali ya hofu inayowakabiri walimu na wanafunzi wa shule ya sekondari Msia kufuatia mlolongo wa matukio ya kihalifu likiwepo la kupigwa risasi na kufa mwanafunzi mmoja mwezi uliopita, Tanzania Daima limegundua.

Hali ya usalama katika shule ya sekondari Msia iliyopo wilayani Mbozi mkoani Mbeya inaendelea kuwa ya wasiwasi kufuatia vitendo vya uhalifu na vitisho vinavyofanywa huku uongozi ukiwa haujui la kufanya.

Wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari hizi aliyefika shuleni hapo wananchi mbalimbali pamoja na walimu waliopo katika shule hiyo, walisema wamekuwa wakiishi maisha ya hofu kufuatia matukio ya uhalifu yanayofanywa na wanafunzi pasipo hatua zozote kuchukuliwa na uongozi wa shule.

Mmoja wa walimu ambaye aliomba jina lake lisiandikwe gazetini alisema wamekuwa wakiishi kwa hofu hali ambayo inapelekea baadhi ya walimu wenzake kutaka kuhama shule ili kwenda mahali pengine ambapo usalama wao utakuwa ni wa uhakika.

Alidai kuwa wamejaribu kujadili hatma ya maisha yao shuleni hapo na kupitisha mapendekezo kadhaa ikiwemo kumuona Mkuu wa Mkoa wa Mbeya John Mwakipesile ili aweze kuwasaidia kutatua matatizo yanayoizunguka shule hiyo baada ya uongozi wa shule na wilaya kushindwa kufanya hivyo.

Wameelekeza lawama kwa Bodi ya Shule hiyo ambapo imeonekana kushindwa kutekeleza majukumu yake na kwamba baadhi ya wajumbe wa Bodi hiyo hawana sifa za kufanya kazi hiyo na wametoa mapendekezo ya kuvunjwa Bodi ya shule hiyo ili iundwe Bodi nyingine ambayo itajenga mahusiano mazuri baina ya shule na wanajamii wanaoizunguka shule hiyo.
Mwalimu huyo akielezea matukio hayo alisema kuwa mwishoni mwa mwaka jana wanafunzi walifanya fujo iliyosababisha uharibifu wa mali kwa kufyeka kahawa na kuharibu saruji na mbolea vyote vikiwa na thamani ya zaidi ya sh. 25 milioni, tukio lingine ni lile la hivi karibuni ambapo mwanafunzi mmoja aliuawa na Polisi wakati akiwa pamoja na watu wengine wasiojulikana walipofika shuleni hapo kwa nia ya kutaka kuvunja na kuiba, lakini kwa bahati nzuri taarifa za ujio wao zilivuja hivyo kupelekea polisi kuweka doria usiku huo.

Pamoja na hayo, walimu hao wameendelea kudai kuwa hivi sasa wamepata taarifa kwamba kuna kikundi kina mpango wa kutaka kuichoma moto shule hiyo taarifa ambazo pia polisi wamezipata, hivyo kwa kuwa matukio yote mabaya yaliyotokea shuleni hapo taarifa za kuwapo kwake ziliwahi kuvuja mapema, wanaamini kuwa hata tukio hilo linaweza kuwa kweli na kwa vile tayari wanawataja baadhi ya walimu kuwa nao watawashambulia kwa kuwa ni kikwazo cha kufanya mambo yao.

Mwananchi mmoja anayeishi jirani na shule hiyo Daudi Simkoko aliliambia gazeti hili kuwa matatizo yanayotokea katika shule hiyo yanatokana na uongozi mbovu ambao haushirikiani na watumishi pamoja na wananchi wengine katika kuimarisha nidhamu ya wanafunzi, kwani matukio haya yanatokana na utovu wa nidhamu kwa wanafunzi.

Alisema hivi sasa baadhi ya walimu wameondoka kwa madai ya kwenda kusoma na kusababisha upungufu mkubwa wa walimu, hali ambayo imesababisha wazazi kuamua kuitisha mkutano utakaofanyika wiki ijayo ili kujadili namna ya kuwapata walimu wa muda ambao watawalipa wenyewe.

Afisa Mtendaji wa kata ya Msia Partson Nsyengula alipoulizwa kama kata yake ina mkakati gani wa kurejesha mahusiano baina ya wanafunzi, walimu na wanakijiji alisema kuwa Kamati ya ulinzi na usalama ya kata imepitisha mapendekezo ya kuongeza ulinzi kwa kuajiri walinzi wengine wanne, pia wamependekeza kununua bunduki badala ya kulinda kwa kutumia marungu.

Nsyengula alikiri kuwa Bodi ya shule hiyo haijawahi kufanya vikao vyake hivyo kuongeza kuwa pengine matatizo yaliyopo yanatokana na kulimbikizwa kwa matatizo mengi madogo madogo.

Mwenyekiti wa Bodi ya shule Francis Mwakabenga alipohojiwa na gazeti hili kuhusu migogoro ya shule hiyo alidai yapo mambo mengi yaliyochangia na kwamba atatoa ufafanuzi wake kimaandishi kutokana na simu yake kuishiwa chaji hata hivyo aliomba muda wa kujipanga ili ajibu maswali ya gazeti hili.

Mkuu wa shule Absolom Mwakyoma alipoombwa kuzungumza na mwandishi wa habari hizi baada ya kumkosa shuleni na kukutana naye njiani aliahidi kuja siku inayofuata kwani siku hiyo alikuwa na haraka.

“hivi sasa niko Busy naelekea Mbeya, hata baadaye nikirudi sitafika hapa nitakwenda kijijini, lakini nitaangalia ili nikutafute” alieleza Mkuu huyo kwa kusisitiza lakini hadi tunakwenda mitamboni hajatokea.

Mratibu wa Elimu ya sekondari wilayani hapa Mathias Lyoto alikiri kuwa migogoro inayoonekana inatokana na matatizo ya kiuongozi na kwamba mapendekezo ya wakaguzi wa shule wa kanda yamepelekwa ngazi za juu kwa kubarikiwa na hatua zaidi likiwepo la kuvunjwa Bodi ya Shule.

Aliongeza kuwa mengi ya matatizo hayo yamekuwepo kwa muda mrefu na kwamba Bodi ilikuwa haifuati ratiba ya kufanya vikao mara nne kwa mwaka kitu kilichofanya matatizo kuwa makubwa.

Uchunguzi zaidi wa gazeti hili umebaini kuwepo kwa makundi matatu katika migogoro hiyo, ambapo kundi moja ni la wanafunzi wanaoungwa mkono na baadhi ya walimu wasioridhika na shule inavyoendeshwa ambapo wamedai inaendeshwa kidikteta na mkuu wa huyo wa shule.

Kundi jingine ni la wanafunzi walio upande wa walimu wanaokubaliana na Mkuu huyo wa shule na hili ndilo lililovujisha habari za kuwepo kwa njama za kutaka kuvunja na kuiba shuleni hapo ambapo walitoa taarifa na polisi wakawahi kujipanga na kumuua mwanafunzi aliyekuja kuvunja kama ilivyoripotiwa na vyombo mbalimbali vya habari.

Kundi la tatu ni la baadhi ya wananchi ambao hawaridhiki na mwenendo mzima wa maendeleo ya shule hiyo wakiwatuhumu viongozi kutafuna michango ya shule na kugomea kuchangia shule nyingine inayojengwa katika kata hiyo ambayo ilimfanya Mkuu wa wilaya Halima Kihemba kumsimamisha uenyekiti wa kijiji Mwashitete miezi miwili iliyopita.

Hata hivyo uchunguzi zaidi umebaini suala la migogoro katika shule hiyo yanabeba pia sura ya kisiasa kufuatia hatua zilizochukuliwa na Mkuu huyo wa wilaya ambapo anadaiwa kutoshirikisha uongozi wa chama tawi la Msia ambalo linaendelea kumtambua Mwashitete kama mwenyekiti halali kwani hakuna taratibu kichama zilizochukuliwa dhidi yake.

MWISHO.

Tuesday, March 4, 2008

MAPIGANO KATI YA WAKULIMA NA WAFUGAJI

Posted by Unknown On 12:48 AM No comments
Na Kenneth Mwazembe
Mbozi.

WANANCHI wa vijiji vya kata ya Myunga wilayani Mbozi mkoani Mbeya wanaishi kwa wasiwasi wakihofia kulipuka kwa mapigano kati yao na jamii ya wafugaji ya Wasukuma waliohamia katika vijiji hivyo, imefahamika.

Hofu hiyo imekuja baada ya kutokea ghasia na mapigano madogo ambapo wakulima wamevamia vibanda na makazi ya wafugaji hao na kuvibomoa na kuchoma moto wakishinikiza wafugaji hao kuondoka katika vijiji vyao.

Kwa upande mwingine, mfugaji mmoja Mwendesha Kitakuja (28) wiki iliyopita alimpiga na kumjeruhi Paulo Simkonda (36) kwa fimbo kichwani katika mapigano yaliyohusisha mashoka na mikuki ambapo viongozi walishinikiza mjeruhiwa kulipwa fedha za matibabu shilingi 160,000 na mjeruhi na kisha viongozi kulipwa shilingi 40,000 za ofisi.

Wakulima hao wakizungumza kwa nyakati tofauti na mwandishi wa habari aliyefika katika vijiji hivyo, wameeleza kutokuwa na imani na viongozi wao kutokana na kuwatuhumu kupokea fedha (rushwa) kutoka kwa wafugaji hao ambako kumewawezesha kupokelewa kijanja katika vijiji vyao.

Aidha wametaja vijiji vilivyokumbwa na zahama hiyo ya wafugaji kuwa ni Ipatikana, Chilangu, Nzoka, Mpui na Myunga ambapo kiini cha mgogoro huo ni usaliti wa viongozi uliobainika ambapo wameelezewa kujinufaisha binafsi kwa kuwepo kwa wafugaji hao.

Wameongeza kuwa wafugaji wanatoa pesa nyingi kuwapa viongozi wa vijiji na kata na kuwapuuza wakulima wanapopeleka malalamiko yao kuhusu uharibifu unaofanywa na mifugo.

Vily Daimon Sichalwe, balozi wa shina na 3 amelalamikia mwenendo mzima wa kuwapokea wafugaji hao na kwamba wao hawana sauti kwa viongozi wao na hakuna ushirikishwaji wala taarifa inayotolewa.

Naye Sadock Simkonda, mkulima wa kijiji cha Myunga aliyepambana na wasukuma kwa kutumia upinde na mishale na kuwafukuza kwenye eneo lake ameeleza kuwa wao wanawalaumu viongozi ambao wameshindwa kuweka utaratibu maalum wa kutenga maeneo ya kilimo na ufugaji na hivyo kuongeza uhasama baina ya pande mbili hizo.

Hali hiyo imewalazimu wakulima wengi kuhamia mashambani kwa msimu huu wa kilimo ili kulinda mashamba yao kutokana na mifugo hiyo.

Sinsco Simpanzye (45) mkulima ambaye shamba lake lilivamiwa na kuisha mwaka jana amelazimika kuhamia shambani msimu huu wa mazao kulinda hadi atakapovuna.

Katika jamii ya wafugaji, Mwendesha Kitakuja ameeleza kuwa yeye amehamia hapo kijijini kwa kukaribishwa na viongozi ambao walimdai kutoa jumla ya shilingi 630,000 kama fedha za kiingilio na mchango wa ujenzi wa shule ya sekondari ambapo yeye ana miliki ngombe 600 na kondoo 40 na kwamba alipohamia hapo kijijini alishauriwa kuoa binti wa wenyeji ili kudumisha mahusiano na kwamba ameoa tayari na kununua shamba la ekeri nane kwa shilingi 210,000 kwa Maiko Simpanzye.

Aidha alieleza kuwa yeye anawaleta ng’ombe wake kwa awamu na kila awamu hudaiwa kulipa fedha za kiingilio, na kwamba yeye anasaidia wanakijiji kwa kuwauzia maziwa.

Naye Masasila Daudi (22) mfugaji mwingine katika kijiji hicho anadai kuwa wao kama wafugaji wamelazimika kuhama kutoka kijiji cha Uzia kata ya Muze tarafa ya Mtowisa wilayani Sumbawanga na kuhamia hapo wakimfuata ndugu yao Mwendesha kwa kuwa yeye anafahamiana na viongozi na kwamba uhamiaji wao siyo mgumu kwani wanatumia jina moja la yule aliyekubalika kijijini hapo.

Viongozi waliotuhumiwa kupokea fedha hizo akiwemo diwani wa kata hiyo Credo Simwinga walipohojiwa kwa simu baada ya kutopatikana kijijini hapo wamekanusha kulipwa fedha hizo na kudai kuwa malipo hayo ni halali kwa kuwa kulikuwa na maelewano maalum.

Kaimu Mtendaji wa kijiji cha Myunga Yohana Simwanza amedai kuwa hali ya kuchukua fedha za wafugaji ni halali kwa kuwa wanachangia maendeleo na kwamba serikali za vijiji hazina mafungu ya kukarimu wageni kutoka wilayani na hivyo kuwalazimu kutumia akili ya kuwaomba jamii ya wafugaji kukidhi haja.

Uchunguzi zaidi umebaini kuwepo mtandao wa upokeaji fedha hizo kuanzia ngazi ya kijiji, kata, tarafa hadi wilayani ambapo jeshi la polisi wilayani hapa wamedaiwa kupokea fedha hizo na wakala aliyetajwa kwa jina moja la Ibrahimu ambaye hupita kwa wafugaji na kuwachangisha ili kujiwekea uhalali wa wao kuendelea kuwepo katika vijiji hivyo.

Baadhi ya viongozi wa kijiji cha Chilangu wamedaiwa kupewa ng’ombe na wafugaji hao na kwamba walipokosana wafugaji hao walidai kurudishiwa ng’ombe hizo na hivyo kuwafanya viongozi hao kuchochea chuki kwa wakulima.

Afisa Mtendaji Kata ya Myunga Mdinde Mdinde alipotakiwa kutoa maelezo juu ya migogoro iliyoikumba kata yake alisema kuwa chanzo ni viongozi wenyewe wa vijiji ambao wametanguliza maslahi yao bila kujali athari zake kwani wafugaji nao wanastahili kuishi katika maeneo hayo kinachotakiwa ni mipango mizuri ya kugawa matumizi ya ardhi.

Aliongeza kuwa tukio la juzi ambalo naye alikamatwa na polisi kwa tuhuma za kumvamia mfugaji lilifanywa na Halmashauri ya kijiji cha Mpui ambapo viongozi wenyewe ndiyo walioongoza operesheni hiyo ya kubomoa vibanda na kuvichoma moto kwa lengo la kuwafukuza wafugaji.

Hata hivyo tathmini ya awali iliyofanywa na mwandishi aliyepita kuona hali halisi katika mashamba yanayodaiwa kufanyiwa uharibifu imebaini kuwepo uharibifu wa kawaida kwa mashamba hayo hali inayoonesha kuwepo kwa sababu nyingine zaidi ya hiyo inayodumisha chuki za chini kwa chini baina ya jamii hizo.

Mkuu wa wilaya ya Mbozi Halima Kihemba akizungumzia migogoro hiyo amesema amewapa maelekezo viongozi wote wa maeneo husika kukaa vikao vya pamoja na kufuata taratibu za kisheria ili wafugaji hao waishi bila kubughudhiwa na kuandaa ramani zitakazo idhinishwa na mamlaka husika.

Site search

    More Text