Tuesday, April 26, 2011

Nimerudi

Posted by Unknown On 6:54 AM No comments
Jamani mwenzenu nilikuwa nimeitikia wito wa Rais wetu Jakaya Mrisho mwana wa Kikwete wa kutekeleza Kilimo Kwanza sina mafanikio najaribu tu
Wafanyabiashara mtatumaliza

MAUAJI yanayoambatana na imani za kishirikina yameibuka na kutia hofu wakazi wa kijiji cha Myunga wilayani hapa na kuwafanya washindwe kufanya kazi za uzalishaji mali.

Matukio yaliyozua hofu ni mauaji ya msichana ambaye hajatambuliwa aliyeuawa Aprili 20 na kutupwa katika mto Lwasho ambapo alikutwa na wavuvi ambao walitoa taarifa kwa uongozi wa kijiji.

Baada ya uchunguzi maiti alibainika kutolewa ulimi, maziwa, meno na sehemu za siri hali iliyoamsha hasira za wananchi na wakawataka polisi kuondoka na mfanyabiashara Kasandilo Mteka ambaye walimtuhumu kuhusika na mauaji hayo.

Hata baada ya polisi kuondoka na mtuhumiwa huyo wananchi hao wenye hasira waliamua kuvunja nyumba ya mtuhumiwa ambapo walipekua na kuvikuta vitu vinavyodhaniwa kutumika katika kazi hizo za mauaji zikiwemo sindano mbili zilizodaiwa kuwa ni za BM.

Ambapo baada ya mahojiano mtuhumiwa alimtaja kamanda wa polisi mkoani Tanga kuwa ndiye mwenye vyombo hivyo.

Wananchi hao walimkamata mtuhumiwa mwingine Leonard Simfukwe na kumpiga hadi kumuua ambaye aliwataja watu wengine kumi wanaojihusisha na mauaji hayo wakiwemo wengine toka mkoani Rukwa na pia alielekeza kuwa kuna miili mingine mitano imefungwa mawe na kutumbukizwa mtoni ikiwa imenyofolewa baadhi ya viungo ambavyo vinauzwa nchini Zambia.

Katika operesheni hiyo alikamatwa mwingine aliyejulikana kwa jina la Tall Siwiti mkazi wa Miangalua mkoani Rukwa ambaye alinusurika kuuawa baada ya polisi kumnusuru na hivi sasa amelazwa katika hospitali ya Laela mkoani Rukwa kufuatia kipigo kikali alichopewa.

Wananchi walioshuhudia tukio hilo walieleza kuwa watuhumiwa hao hawajaonewa bali mwenendo wao na kazi wanazozifanya ndizo zinawashitaki na kwamba si hao tu bali kundi lote linahitajika kukamatwa na polisi na kama watashindwa basi wao watachukua hatua stahili.

Aidha hali si shwari kabisa eneo hilo kufuatia baadhi ya watuhumiwa waliotajwa kutoroka na kuziacha familia zao wakiwemo wafanyabiashara wa eneo hilo ambapo mmoja wao aliyejulikana kwa jina moja la Simundwe alihamishwa chini ya ulinzi wa polisi.

Afisa Mtendaji wa kijiji cha Myunga Edwin Sikapizye alithibitisha kutokea kwa matukio hayo na kwamba wanasubiri hatua za polisi za uchunguzi ikiwemo utafutaji wa miili hiyo mitano iliyozamishwa mtoni baada ya kuuawa.
Mwisho
HUJUMA nzito zimefanywa dhidi ya chuo cha uuguzi na ukunga cha Mbozi kilichopo wilayani Mbozi mkoani Mbeya zilizosababisha hasara kubwa na kuzusha wasiwasi miongoni mwa jamii inayokizunguka chuo hicho.

Akizungumza na waandishi wa habari waliofika chuoni hapo jana mkuu wa chuo hicho Hiza alieleza kuwa matukio yaliyotokea mfululizo ni pamoja na kutiwa chumvi kwenye injini ya gari STK 3014 aina ya Land Cruiser Machi 14 mwaka huu na kusababisha gari hilo kuharibika.

Tukio la pili ni kuchomwa moto kwa ofisi ya mkuu wa chuo ambapo mali nyingi na nyaraka muhimu ziliteketea zikiwepo kompyuta kubwa 2, laptop 2, photocopy 1 pamoja na samani zilizokuwemo humo ambapo thamani halisi ya mali iliyoharibika bado haijafanywa na mthaminishaji wa serikali.

Pamoja na mambo hayo pia mkuu huyo ameeleza kuwa anaishi kwa hofu kufuatia vitisho anavyopewa ikiwa ni pamoja na kulazimishwa kumteua msaidizi wa mkuu wa chuo ambao wafanyakazi walio wengi walimtaka.

“Nilivyofika hapa mwaka jana Februari wafanyakazi wa ngazi ya chini walikuwa wakinijia mara kwa mara kunitaka nimteue mmoja wa walimu (jina limehifadhiwa) kuwa msaidizi wangu lakini nilikaa kimya nikiangalia ni nani ningemteua ndipo nilipomteua Josephat Kaja kuwa msaidizi wangu na hapo ndipo nilipopokea barua ya kunipa siku 14 nibatilishe uamuzi vinginevyo wangenifanyizia” alieleza mkuu wa chuo.

Baadhi ya wafanyakazi chuoni hapo ambao waliomba majina yao kuhifadhiwa walisema kuwa chanzo cha mgogoro huo ni mfumo wa uongozi ambapo walidai kuwa tangu aje mkuu wa chuo huyo mgeni pamekuwepo mabadiliko makubwa ya namna ya kudhibiti mali ya chuo na kwamba uhuru uliokuwepo wa kufanya watakavyo ulikwisha.

“ Nenda kwenye bwalo la chakula kumenunuliwa viti vipya zaidi ya mia tatu, kumepakwa rangi na kuwekwa marumaru mambo hayo yamefanywa na mgeni huyu ambaye amemaliza mwaka sasa” aliongea mfanyakazi huyo.

Hata hivyo wananchi wameomba kuitishwa kwa mkutano ambapo wanatarajia kupiga kura za kumtaja anayehujumu chuo hicho mbele ya mkuu wa wilaya ya Mbozi na kwamba watamtaka mkuu wa wilaya kuondoka naye mara baada ya kura hizo.

Sungusungu wanapolizidi Jeshi la polisi

Posted by Unknown On 6:43 AM No comments
JESHI la Polisi wilayani Mbozi mkoani Mbeya limeingia katika kashfa kiutendaji baada ya kuibuka kundi la watu linalofanya vitendo vya kihalifu ikiwepo mauaji ya watu na kuwafanya wananchi wa kata za Itaka, Bara, Nambinzo na Halungu wilayani hapa kuishi kwa hofu.

Kundi hilo ambalo limeanzishwa miezi mitatu iliyopita linalojulikana kwa jina Shulu ikiwa na maana ya kichuguu (lugha ya Kinyiha) na kuwa ni sungusungu wa polisi jamii na kwamba linafanya kazi hizo kwa lengo la kukomesha vitendo vya kihalifu.

Watu waliotajwa kuuawa na kundi hilo ni Saison Mtajiha wa kijiji cha Hangomba ambaye alikamatwa na silaha na Potea Vileji wa kijiji cha Hamwelo na mwingine ambaye jina lake halikuweza kupatikana mkazi wa kijiji cha Utambalila aliyedaiwa kuiba kuku.

Waliopigwa na kujeruhiwa ni Daudi Mwashitete ambaye amevunjwa miguu yote miwili na mkono na amelazwa katika hospitali ya Vwawa, wengine ni Lidia Shinanga, Misheki Msumeno na Weki Jamson wakazi wa kijiji cha Hangomba na Adimin Mdalavuma wa kijiji cha Bara.

Mmoja wa watu aliyepigwa na kuvunjwa miguu yote miwili na mkono mmoja Daudi Mwashitete akiwa amelazwa katika hospitali ya wilaya ya Mbozi mjini Vwawa alisema kuwa yeye alikamatwa kwa tuhuma za wizi wa mashine ya kukoboa kahawa aliyokuwa amewekeza rehani kwa Yela Mwalupogo.

“Walinifuata shambani na kunikamata na kunipeleka kilabuni ambako nilihojiwa juu ya mashine ya kukoboa kahawa ambayo waliikuta kwa Mwalupogo wakidhani ni mali ya wizi, niliwathibitishia kuwa hiyo ni mashine yangu halali niliyowekeza rehani ili kulipa deni la pembejeo za kahawa la sh 80,000 nilizokopa kwa Julius Mgala lakini hawakunielewa na ndipo walipoanza kunipiga kwa marungu na kunivunja miguu yangu yote na mkono huu wa kulia” alisema kwa uchungu.

Mwashitete aliwataja waliokuwa wakimpiga kuwa ni Japhet Halinga, Peter Howa, Harrison Mwashilindi, Tusoweye Mnkondya na mwingine aliyetajwa kwa jina moja la Nambwama.

Hata hivyo katika hali isiyokuwa ya kawaida sungusungu hao walifika katika hospitali na kumtorosha majeruhi Daudi Mwashitete na kumpeleka kwa mganga wa kienyeji katika kijiji cha Nambinzo ili atibiwe huko na kuondoa ushahidi wa hospitali lakini baada ya majeruhi kupata fahamu alituma ujumbe kwa ndugu zake ambao walimrudisha hospitalini hapo.

Kiongozi wa kikundi hicho Japhet Halinga (au Ngwede) alipohojiwa kwa simu namba 0754 050 667 alikiri kuwakamata watuhumiwa waliotajwa kupigwa akidai kuwa anafanya kazi hizo kwa maagizo ya polisi na kwamba matukio yote hutolewa taarifa zake katika kituo cha polisi Itaka.

“Sisi tukiwakamata huwalazimisha watuoneshe mali walizoiba na wakisumbua ndipo vijana wetu huwashughulikia kama ulivyoona” aliongeza Halinga.

Hata hivyo baadhi ya wananchi wametajwa kuwa wamekamiwa kuadhibiwa na kikundi hicho na wameshatoa taarifa hizo katika kituo cha polisi Itaka ambapo hakuna hatua zilizochukuliwa hadi sasa.

Wananchi hao waliozungumza na mwandishi wa habari hizi ni Langford Philimon, Yangson Shinanga, Williad Mwashilindi, Anjelo Simfukwe, Chilumba Philimon, Oyes Mgala na Juma Mgaya. Wamedai kuwa wamekuwa wakipewa vitisho vya mara kwa mara kwamba siku yao bado inakuja.

Watu hao wameeleza kuwa wanapopeleka malalamiko yao katika kituo cha polisi huambiwa wakatoe taarifa hiyo kwa mwenyekiti wa sungusungu (SHULU) ndiye atakayeshughulikia matatizo yao.

Baadhi ya wananchi walisema hatua ya kukamata wahalifu hatupingi tatizo ni pale wanapowapiga na kuwafanya vilema hapo wanaongeza tatizo kwa taifa. Wameongeza raia hao kuwa kundi hilo likikukamata ukiwa na shilingi 200,000 linakudai ukiwapa wanakuachia ila kama kuna mali ulizokamatwa nazo wanazichukua.

Mkazi mwingine aliyeomba kuhifadhiwa jina lake anasema watu wote walioorodheshwa kukamatwa wanatakiwa angalau kuwa na shilingi 100,000 kama kima cha chini ili ukikamatwa wasikupige kufuatia tishio hilo baadhi ya wananchi wanakimbia wakiziacha familia zao.

Joseph Mwanakulya mkazi wa kijiji cha Itaka akitoa maoni yake juu ya kundi hilo alisema mali za wizi zinakamatwa watu waliopotelewa vitu vyao wanavipata shida ni hivyo vilema wanavyowatia watu pengine wangerekebisha kipigo tungewaona wanafaa.

Nako katika kijiji cha Halambo kata ya Halungu sungusungu hao wamewapiga na kuwajeruhi vibaya Wilinasi Sikanyika na mtoto wake Stephano Wilinas ambao wanapata matibabu katika hospitali ya Vwawa, mtoto akiwa na tuhuma ya kuiba ng’ombe miaka mitatu iliyopita ilihali baba yake alipigwa kwa tuhuma za kutaka kumsaidia mtoto wake ambaye alipeleka malalamiko katika kituo cha polisi mjini Vwawa.

Afisa Mtendaji wa kijiji cha Hangomba Watson Maduguli alipoulizwa juu ya kundi hilo alikiri kuwepo na kwamba kazi wanazofanya hajui utaratibu wake lakini anadhani wilaya inajua. Alipohojiwa juu ya uongozi wa kundi hilo alionekana kujibu kwa mashaka na akaomba apewe muda wa kufuatilia na kwamba anachojua ni kukamatwa kwa watu na kuadhibiwa.

Naye mwenyekiti wa kijiji cha Utambalila Francis Nzowa alipohojiwa juu ya kuwepo kwa mauaji kijijini kwake alisema kuwa mtu aliyeuawa aliiba kuku lakini taarifa za kifo chake zilipelekwa polisi.

Afisa mtendaji wa kijiji cha Hamwelo Osia Mgala alipohojiwa juu ya mauaji ya Potea Vileji alijibu kuwa huyo aliiba mablanketi ndipo akaadhibiwa na wananchi.

Mganga Mkuu wa hospitali ya wilaya Nicolaus Mbilinyi alithibitisha kuwapokea majeruhi wawili Admin Mdalavuma ambaye ametibiwa na kuruhusiwa na Daudi Mwashitete ambaye alisema anapelekwa katika hospitali ya rufaa jijini Mbeya kufuatia mivunjiko ya miguu na mkono ambapo hawataweza kumtibu katika hospitali yake.

Mkuu wa wilaya ya Mbozi Gabriel Kimoro alipohojiwa juu ya kuwepo kwa kundi hilo alidai kuwa hana habari na kwamba ndiyo kwanza anapata habari kupitia mahojiano hayo.

Mkuu wa polisi mkoani hapa Advocate Nyombi alipohojiwa juu ya kuwepo kwa kundi hilo na vitendo hivyo vya kinyanyasaji vinavyofanywa alikanusha kuwa na taarifa yoyote juu ya kundi hilo na kwamba atafanya uchunguzi.

Hata hivyo polisi hawajachukua hatua yoyote kwa wahusika walio wajeruhi watu hao pamoja na taarifa kupelekwa katika vituo vya polisi vya Itaka na Vwawa hali inayofanya wananchi waishiwe imani na jeshi hilo.

Site search

    More Text